JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA NISHATI NA MADINI
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
UENDELEZAJI WA MRADI WA KUUNGANISHA GRIDI ZA UMEME ZA ZAMBIA-TANZANIA NA KENYA (ZTK)
Napenda kuwajulisha kwamba Wizara ya Nishati na Madini itakuwa mwenyeji wa Mkutano wa Mawaziri wa Nishati wa wa nchi za Zambia, Kenya na Tanzania unaotarajiwa kufanyika tarehe 30 Septemba, 2014 ambapo Wizara ya Nishati na Madini itakuwa mwenyeji wa mkutano huo utakaofanyika katika hoteli ya JB Belmonte jijini Dar es Salaam.
Mkutano huo utajadili juu ya utekelezaji wa mradi wa kuunganisha mtandao wa umeme katika gridi za nchi hizo tatu (Zambia, Tanzania, Kenya) ‘ZTK power interconnector project).
Aidha, Mkutano huo utatanguliwa na mikutano ya Makatibu Wakuu tarehe 29 Septemba, 2014 na mkutano wa wataalam wa sekta ya Nishati ya umeme kutoka nchi hizo tatu.
Katika mkutano huo, Mashirika ya umeme kutoka katika nchi hizo zitawasilisha taarifa za utekelezaji wa miradi ya kuunganisha mtandao wa umeme pia watajadili na kusaini mkataba wa makubaliano ya utekelezaji wa mradi (Heads of Agreement – HOA).
Mwaka 1995, Mashirika ya umeme ya Zambia, Tanzania na Afrika Kusini yalianza kufanya upembuzi yakinifu kwa ajili ya kutathimini uwezekano wa kuunganisha mifumo ya gridi za umeme za Zambia na Tanzania. Upembuzi huo ulikamilika mwaka 1998 na kuthibitisha kuwa kuunganishwa kwa gridi za nchi husika kuna faida za kiuchumi, kijamii, kiufundi na kifedha.
Mwezi Januari, 2001, Mawaziri wanaosimamia masuala ya Nishati wa Zambia, Tanzania na Kenya walikutana ambapo Serikali ya Kenya ilionesha nia ya kushiriki katika mchakato wa kuendeleza mradi kwa lengo la kupata fursa ya kununua umeme wa bei nafuu kutoka Zambia. Hali hii ilibadili upeo wa mradi na kujulikana kama Zambia -Tanzania - Kenya Power Interconnector Project. Mradi huu unahusisha sehemu kuu zifuatazo:
i. Ujenzi wa laini ya msongo wa 400kV yenye uwezo wa kusafirisha MW 400 kutoka kituo cha kupoozea umeme kilichopo Pensulo, Zambia hadi kituo cha kupoozea umeme cha Mwakibete, Mbeya kwa upande wa Tanzania,
ii. Kuimarisha mfumo wa usafirishaji umeme nchini kwa ajili ya kuwezesha kusafirisha umeme unaotosheleza, wenye ubora na uhakika katika maeneo ya kaskazini, kaskazini mashariki na magharibi hadi kufikia Kenya kwa kujenga njia mpya ya kusafirisha umeme kutoka Mbeya hadi Singida katika msongo wa kV 400, na
iii. Ujenzi wa laini ya kusafirisha umeme yenye msongo wa kV 400 kutoka Arusha hadi Nairobi
Aidha, mradi wa ZTK ni mmoja kati ya miradi ambayo kwa siku nyingi imekuwa katika Mpango Kabambe wa Kuendeleza Sekta ya Umeme (PSMP) kama miradi mhimili ambayo kuendelezwa kwake kutachangia kuwepo kwa vyanzo vya umeme mbadala kutoka nchi za jirani na hivyo kupunguza kwa kiasi kikubwa kero ya upungufu wa umeme ambayo imekuwa ikiikumba nchi yetu mara kwa mara ambayo imesababisha kutoa huduma ya umeme kwa mgawo. Aidha, mradi huu pia utafungua uhusiano wa kibiashara kati ya makampuni ya umeme ya nchi wanachama kwani mifumo ya usafirishaji umeme imepangwa iwe na uwezo wa kusafirisha umeme pande mbili (bi-directional) kwa ajili ya kununua na kuuza umeme kupitia masoko ya East African Power Pool (EACPP) na Southern African Power Pool (SAPP).
Kuunganisha gridi za umeme za nchi jirani ni moja ya mkakati wa kipaumbele ili kuepuka matatizo ya nchi moja kukosa umeme wakati nchi ya jirani inao umeme wa ziada kama ilivyoainishwa katika Power System Master Plan (PSMP). Aidha, ni moja kati ya malengo ya shirikisho la NEPAD kuona kuwa nchi za kusini mwa jangwa la Sahara zinakuwa na ushirikiano wa karibu katika masuala ya kuinua uchumi ambapo huduma ya umeme wa uhakika inahitajika.
Imetolewa na;
Badra Masoud
Msemaji,
Wizara ya Nishati na Madini