Mkutano wa kwanza wa Baraza la Nne la Wafanyakazi wa Taasisi ya Tiba ya Mifupa, ajali na upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (MOI) leo Septemba 23,2018 umefikia tamati kwa wajumbe wa mkutano huo kupitisha maazimio 11 ya kimkakati.
Mkutano huo umehitimishwa na Mwenyekiti wake Dkt. Respicious Boniface ambaye pamoja na mambo mengine amewashukuru wadau walioshirikiana na MOI katika maandalizi ya Baraza hilo na pia kuwapongeza na kuwashukuru wajumbe kwa kushiriki kikamili kwa kuchangia mada mbalimbali zilizowasilishwa na kutengeza maazimio ya kuboresha huduma za Taasisi.
Kwa upande wake Katibu mpya wa Baraza hilo Bwana Ngina Mitti amefurahishwa na ushirikiano ambao ameupata kutoka kwa wajumbe wa Baraza hilo ambapo pia wamemwahidi kuendelea kushirikiana nae katika kuboresha huduma za Taasisi.“Tumemaliza kikao cha kwanza cha baraza la nne la wafanyakazi MOI leo tukiwa na maazimio 11 ambayo nikiwa kama katibu natakiwa kuhakikisha maazimio hayo yanatekelezwa kabla ya kikao cha pili ambacho kitafanyika kabla ya bajeti ijayo.
Kwa ushirikiano mzuri niliouona kutoka kwa Mkurugezi Mtendaji, wakurugenzi wengine, wakuu wa vitengo na wafanyakazi kwa ujumla ni imani yangu kuwa kila kitu kitatekelezwa kwa wakati kwa manufaa ya taasisi na taifa kwa ujumla” ameeleza Katibu huyo mpya Bwana Ngina Mitti.
Maadhimio hayo yamelenga kutoa huduma za Afya kwa Watanzania ili kuahakikisha huduma zote za matibabu ya mifupa, ubongo, mgongo na mishipa ya fahamu zinatolewa hapa nchini na kumaliza kabisa rufaa za nje ya Nchi pia kuhakikisha wagonjwa wanaofika MOI wanapata huduma bora na kwa wakati.
Akifunga vikao vya Baraza hilo, Dkt. Boniface amesema Taasisi ipo kwenye mpango kabambe wa kuboresha huduma hususani kwenye upande wa utunzaji wa kumbukumbu kwenye mfumo maalum (Data Base). “Tunataka tuanzishe ‘propper data base’ ya uhakika yaani kila anayeingia anajulikana na anaonekana ili kuondoa ili suala la wagonjwa kuwahi namba hapa ambapo wanakuja kuanzia saa 12 alfajili hii sasa itakoma.
Mfumo huu utasaidia sana hivyo kwa sasa tunajipanga kwa hilo” alimalizia Dkt. Boniface.
Baraza hilo la Wafanyakazi limehudhuliwa na wajumbe zaidi ya 70 huku pia pia wadau mbalimbali wakiwemo SSRA ambao walitoa mada juu ya kuunganishwa kwa mifuko ya hifadhi ya Jamii sambamba na Benki ya NMB ambao ni waadu wakubwa wa MOI ambao walitoa elimu na mafunzo namna ya benki hiyo inavyoweza kuwasaidia wateja wake wakiwemo wafanyakazi wa MOI.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Tiba ya Mifupa, ajali na upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (MOI) Dk Respicious Lwezimula Boniface (Kulia) ambaye alikuwa mgeni rasmi akimpongeza na kumkaribisha Katibu mpya wa Baraza la Wafanyakazi wa MOI, Bwana Ngina Mitti baada ya kuchaguliwa kwenye Baraza hilo la Nne.