Mkurugenzi wa TIB, Charles Singili akipewa maelezo na wafanyakazi wa kampuni ya Alko Vintages kuhusiana na mvinyo wa Dodoma. Katikakati ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano, Sarah Majengo akifuatiwa na Dr Hildebrand Shayo, Meneja wa Mipango na Utafiti.
Afsa Mauzo wa kampuni ya Pipe Industries, Ignas Mafita (kushoto) akimpa maelekezo Mkurugenzi Mtendaji wa TIB, Charles Singili (kulia) juu ya bidhaa zinazozalishwa na kampuni hiyo. Anayetazama katikati ni afsa wa TIB.
Benki ya TIB imepongezwa na wadau mbalimbali kwa jitihada zake kusaidia wajasiriamali wakati wa maonyesho ya kimataifa ya kibiashara yanayoendelea ya Saba Saba.
Benki imetoa fursa kwa baadhi ya wateja wake kutangaza bidhaa na huduma zao katika banda la benki hiyo lilipo katika viwanja vya Sabasaba.Miongoni mwa wateja wake waliopata fursa ya kutangaza biashara katika banda la benki hiyo ni kampuni ya Pipe Industries ambao ni wazalishaji wa mabomba mbalimbali ya kilimo cha umwagiliaji, maji taka na gesi na kampuni ya Alko Vintages ambao ni wazalishaji maarufu wa mvinyo aina ya 'Dompo' .
Benki ya TIB pia inatoa mafunzo ya bure kwa wajasiriamali katika banda lake katika maeneo ya usimamizi wa fedha, masoko, pamoja na utawala.Akizungumza katika banda la benki hiyo, Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa TIB, Bwana Charles Singili, alisema ushiriki wao katika maonyesho ya Sabasaba mwaka huu unaendana na kauli mbiu ya maonyesho ya Sabasaba ambayo yamelenga kuunganisha uzalishaji na masoko.
'Kupitia huduma yetu ya mikopo ya viwanda tumeweza kusaidia makampuni na miradi mbalimbali ikiwemo miradi ya kusindika mazao, miradi ya madini, na ya viwanda, mfano mzuri ni haya makampuni yaliyopewa fursa ya kutangaza bidhaa zao kwenye banda letu la TIB’ alisema Singili.
Akielezea zaidi ushiriki wa TIB, Singili alisema benki yake imejikita katika kusaidia ukuaji wa viwanda na kuwezesha viwanda vidogo vidogo na vya kati ili kuzalisha bidhaa bora zitakazowapatia soko la uhakika ili kusaidia kukuza uchumi wa nchi.