WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amesema Serikali ina kazi kubwa ya
kushughulika na kundi dogo linalojihusisha na lugha za uchochezi wa
kidini ambao unachangia kudhoofisha amani ya nchi.
“Tunajua nia yao ni kufanya nchi isitawalike lakini sisi tumesema
hatukubali. Tumekubaliana na Waziri wa Mambo ya Ndani, ulinzi uimarishwe kila mahali, mshingae kuona watu wanawahoji lakini nia njema, ya kurudisha amani yetu,” alisema Waziri Mkuu.
Ametoa kauli hiyo leo mchana (Ijumaa, Mei 10, 2013) wakati
akiwasilisha salamu za rambirambi kwa niaba ya Serikali wakati wa
ibada ya mazishi ya waumini watatu wa Kanisa la Mt. Joseph Mfanyakazi,
Parokia ya Olasiti, jijini Arusha waliofariki dunia kutokana na
mlipuko wa mabomu uliotokea Jumapili iliyopita, Mei 5, mwaka huu
kanisani hapo.
Waziri Mkuu amewaomba wanachi kutoka ushirikiano kwa vyombo vya dola
kwa kutoa taarifa zozote zitakazosaidia kwenye upelelezi wa tukio
hilo.
“Ninawaomba Watanzania tushirikiane kuwafichua watu hawa waovu kwa
sababu tunaishi nao, ni watu ambao wako miongoni mwetu... Tusaidieni
kutunong’oneza ili tuchukue hatua, alisema.
Waziri Mkuu alisema yeye ni miongoni mwa watu wanaoamini kwamba
ukristo au uislamu hauwezi kuondolewa kwa kuwaua viongozi wa dini au
waumini wao. “Ni kujidanganya tu mtu akiamini kuwa akimuua Askofu,
Mufti au Muumini ataimaliza dini yoyote. Madhehebu haya mawili ni
nguzo kubwa kwa Taifa letu, tunatamani tuendelee kuwa na amani
iliyokuwepo siku zote,” alisisistiza.
Alisema Serikali kupitia idara ya maafa itatoa sh. milioni 100/- ili
zisaidie kukabiliana na janga lililowakabili wana Arusha.
Mapema, akiongoza ibada hiyo, Muadhama Polycarp Kardinali Pengo
aliwataka waumini wote kutolipa uovu kwa uovu bali watende wema ili
kusahihisha maovu. “Ishara ya uovu imetendwa na hawa watu dhidi ya
waumini wenzetu kwa madhumuni yanayojulikana na wao tu bila kuchokozwa
na hawa marehemu ama wale waliko hospitali (majeruhi),” alisema.
“Uovu umeshatendwa, je sisi tufanye nini? Angekuja hapa kanisani yule
aliyesababisha mauti haya, tungemfanya nini?” Alihoji Kardinali Pengo
na kujibiwa na mamia ya waumini waliohudhuria ibada hiyo:
“Tungemsamehe.”
Aliwasihi waumini wote kuendelea kuliombea Taifa la Tanzania ili tukio
hilo na lile la kuuawa kwa Padre Evarist Mushi kule Zanzibar yasiwe
sababu ya kusambaratika kwa amani ya Taifa hili.
“Tusilipe ubaya kwa ubaya, tuendelee kuomba Mungu asikie sala yetu na
awazindue wenye mamlaka watimize wajibu wao,” alisema.
Naye Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT),
Dk. Alex Malasusa akitoa salamu za rambirambi kwa niaba ya Jukwaa la
Wakristo Tanzania (TCF), alilaani waliosababisha mauaji hayo na kusema
kitendo hicho kimelitia doa Taifa kwa vile ni kitendo kinachoashiria
kuchafua amani ya Tanzania.
Aliwasihi waumini wote kutokuwa waona katika kazi ya kumtanga za
Kristo. “Risasi zinapigwa, mioto inayowashwa katika makanisa yetu na
mabomu yanayolipuliwa yasiwe sababu ya kututia hofu. Imani yetu haiko
katika miili bali iko mioyoni mwetu,” alisema.
Askofu Mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo Kuu la Arusha akitoa shukrani kwa
niaba ya Kanisa Katoliki aliwashukuru wote waliofika kuwafariji
kutokana na tukio hilo na kuwathibitishia kuwa kama Kanisa wameguswa
na moyo waliouonyesha.
“Tupige goti, ndiyo kazi tuliyonayo. Tupige goti ili Mungu awafichue
hawa watu, aufichue mfumo wao wa kiovu, na awape nguvu viongozi wetu
wao ni kama sisi na iko siku watatoa hesabu mbele ya Mwenyezi Mungu,”
alisema.
Aliwasihi waumini wote kutoogopa na kuendelea kuomba ili waliohusika
na uovu huo Mungu awafichue na kuwaonyesha hadharani. “Ninaambiwa
msiogope, hakuna kutishwa kwa namna yoyote tunaposimama na Kristo...
sisi hatupaswi kuogopa kwa sababu Kristo alishinda mauti,”
alisisitiza.
Watu 66 waliathirika kutokana na mlipuko huo uliotokea Mei 5, mwaka
huu ambapo watatu wamefariki dunia na kati ya wagonjwa 63 waliobakia,
wanane walihamishiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili, wengine waliotibiwa
na kuruhusiwa kurudi nyumbani, na baadhi wanaendelea kupatiwa matibabu
mjini Arusha.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
IJUMAA, MEI 10, 2013.