Mgeni rasmi Katibu Mtendaji Baraza la Vijana Zanzibar Khamis Faraji Abdalla akizindua Jumuiya ya watanzania wasio na ajira (TUEPO) katika Ukumbi wa Water Front Rahaleo Mjini Zanzibar. Picha na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar.
Mwenyekiti wa TUEPO Ussi Said Suleiman akimtoa maelezo mafupi ya Jumuiya hiyo na kumkaribisha mgeni rasmi kufungua mkutano huo.
Muongozaji wa Mkutano wa Uzinduzi wa Jumuiya ya Vijana wasio na ajira Tanzania TUEPO Msabah Ali Msabah akitoa maelezoa kwa washiriki wa Mkutano huo uliofanyika Ukumbi wa Water Front Rahaleo Mjini Zanzibar.
Picha ya pamoja ya viongozi wa Jumuiya ya TUEPO wakiwa pamoja na Katibu Mtendaji Baraza la Vijana Zanzibar (suti nyeusi) baada ya kufungua mkutano huo. Picha na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar.
Mwenyekiti wa TUEPO Ussi Said Suleiman akiagana na Katibu Mtendaji Baraza la Vijana Zanzibar Khamis Faraji Abdalla.
……………………………………………………………………….
Na Maryam Kidiko / Rahma Khamis Maelezo Zanzibar
Katibu Mtendaji Baraza la Vijana Zanzibar Nd. Khamis Faraji Abdallah amewataka Vijana kujiunga katika Taasisi zitakazo wawezesha kuwainuwa kimaisha.
Hayo ameeleza katika Ukumbi wa Water front Raha leo wakati alipokuwa akizindua Jumuiya ya vijana wasio na ajira Tanzania (Tanzania unemployed people organization) TUEPO .
Amesema Baraza la Vijana Zanzibar lipo kwa ajili ya kuwasikiliza na kuwaelekeza vijana ambao hawana ajira ili waweze kujiendeleza na kujiimarisha katika shughuli mbali mbali za maendeleo ili waweze kujiari wenyewe .
“ Ni lazima tufanye kazi kwa pamoja ili Baraza la Vijana Zanzibar liweze kuimarika na kufanyakazi kwa ufanisi,” aliesema Katibu Khamis.
Akizungumzia lengo la Baraza hilo amesema ni kuwawakilisha Vijana kufaidika na fursa zilizopo, kuwawezesha kujielewa, pamoja na kuwashajiihisha kuwa na uwezo wa kuzalisha mali.
“Ni vizuri kushirikiana pamoja ili vijana waweze kuimarika katika maisha yao na Jamii kwa ujumla,” amesisitiza Khamis Faraji.
Katibu huyo amewapongeza wanajumuiya hao kwa kufanikisha kuanzisha taaluma mbali mbali ikiwemo Ubaharia, Udereva, ushoni, Mapishi pamoja na kusomesha lugha ya kiengereza ambayo lengo lake ni kuwawezesha vijana kuajirika katika Hoteli mbalimbali za ndani na nje ya nchi.
“Tutumie fursa iliyopo kwa ufanisi zaidi bila ya kujali itikadi ya vyama vya siasa,” ameongeza Khamis Faraji.
Nae Mwenyekiti wa Jumuiya ya TUEPO Ussi Saidi Suleiman amesema wanatarajia kuwapatia mafunzo ya ubaharia vijana watatu, vijana 15 mafunzo ya mapishi, kumi ushoni na vijana 20 wanatarajiwa kusomeshwa lugha ya kiengereza.
Mwenyekiti huyo ameiomba Serikali kuwapatia mikopo ambayo itawawezesha vijana kuwaendeleza katika kukuzi vipaji na kujiendeleza kiuchumi sambamba na kuanzishwa viwanda ili vijana waweze kupata ajira.
Jumuiya hiyo imeanzishwa mwezi uliopita na ina wanachama 73 hadi hivi sasa. IMETOLEWA NA IDARA YA HABARI MAELEZO -ZANZIBAR