Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Mhandisi Ngosi Mwihava akifungua kikao kazi hicho
Mtaalamu mwelekezi kutoka Norway Bw. Farouk Al Kasim akiwasilisha mada
Mtaalamu mwelekezi kutoka Norway Bw. Farouk Al Kasim akiwasilisha mada.
========= ======= ======
Wadau kutoka Taasisi za Serikali waanza kupitia rasimu ya kwanza ya sera ya petroli.
Na Greyson Mwase, Bagamoyo
Wadau mbalimbali kutoka taasisi za serikali wameanza kupitia rasimu ya kwanza ya sera ya petroli katika kikao kazi kilichofanyika katika hoteli ya Millenium Sea Breeze iliyopo huko Bagamoyo.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao kazi hicho Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Mhandisi Ngosi Mwihava amesema kuwa, kikao hicho ni maalum na muhimu kwa ajili ya kupata michango ya wadau hao ili kuboresha rasimu ya sera ya petroli.
Mhandisi Mwihava aliongeza kuwa awali rasimu hiyo iliandaliwa na timu maalumu kwa kushirikiana na mtaalam mwelekezi kutoka Norway Bw. Farouk Al Kasim. Timu hiyo ilijumuisha watalamu kutoka Wizara ya Nishati na Madini, Ofisi ya Rais –Tume ya Mipango, Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Nishati na Maji Zanzibar, Shirika la Maendeleo ya Petroli Nchini (TPDC) Mamlaka ya Mapato Nchini (TRA) na Baraza la Usimamizi wa Mazingira (NEMC)
Mhandisi Mwihava aliongeza kuwa lengo la kamati iliyoundwa lilikuwa ni kuandaa rasimu ya sera itakayolenga maeneo yote muhimu yanayohusiana na sekta ya petroli.
Mhandisi Mwihava alisisitiza kuwa wakati wa uandaaji wa sera hiyo, kamati ilipitia sera za petroli za nchi nyingine kama Norway, Uganda, Ghana, Sierra Leone, Pakistan ili kupata uzoefu.
Alisema pia kamati hiyo ilitembelea nchi ya Norway ikiwa ni pamoja na kufanya majadiliano ya kina na taasisi za serikali ya Norway zinazosimamia sekta ya petroli ikiwa ni pamoja na kupitia sera zake kwa ajili ya kuongeza ujuzi na uzoefu.
Aliongeza kuwa sera hii itatumika kama msingi wa kuboresha usimamizi wa sekta ya petroli ikiwa ni pamoja na sheria na kanuni, uendelezaji wa taasisi husika ikiwa ni pamoja uendelezaji wa mpango mkakati wa kukuza uchumi wa nchi.
Mhandisi Mwihava alitumia nafasi hiyo kuishukuru serikali ya Norway kwa ushirikiano iliyoonesha kwa nchi ya Tanzania katika uandaaji wa sera ya petroli.
Wakati huo huo mtaalam mwelekezi kutoka Norway, Bw. Farouk Al Kasim akiwasilisha mada alisema kuwa sera ya petroli inahitaji umakini mkubwa sana huku ikishirikisha wadau mbalimbali.
Bw. Kasim alisema mambo yanayotakiwa kugusiwa kwenye sera ya petroli ni pamoja na mkakati wa usimamizi, ushirikishwaji wa wananchi, uwekezaji kwenye mafunzo kwa wazawa ikiwa ni pamoja na fursa za uwekezaji.
Akielezea changamoto katika sekta ya petroli kutokana na uzoefu wake kwa nchi zilizoanza uchimbaji wa petroli Bw. Kassim aliongeza kuwa kumekuwepo na taarifa zinazopotoshwa na baadhi ya watu kwa ajili ya maslahi fulani, kutoa matumaini makubwa zaidi ya matarajio ya wananchi, kuingia mikataba mibovu na wawekezaji, usimamizi mbovu ikiwa ni pamoja na kutokuzingatia usalama wa mazingira.
“Ndugu zangu uandaaji wa sera ya petroli unahitaji umakini mkubwa sana, kwani ni sekta inayoweza kutajirisha nchi ikisimamiwa ipasavyo, ikisimamiwa vibaya inaweza kugeuka kuwa laana badala ya baraka.” Alisisitiza Bw. Kasim.
Naye Kamishna wa Nishati na Maendeleo ya Petroli Mhandisi Hosea Mbise alisema kuwa kutokana na kuongezeka kwa kasi ya utafutaji wa mafuta na gesi umepelekea serikali kuandaa sera ya petroli.
Mhandisi Mbise aliongeza kuwa sera hiyo inalenga uendelezaji wa maeneo ya utafutaji na uchimbaji wa petroli, usimamizi wa sekta ya petroli, sheria ikiwa ni pamoja na usimamizi wa mazingira. Mhandisi Mbise aliongeza kuwa serikali imeanza kupeleka wataalamu nje ya nchi kama moja ya maandalizi ya usimamizi wa sekta ya petroli.