Quantcast
Channel: JIACHIE
Viewing all 46202 articles
Browse latest View live

WAZIRI WA AFYA ZANZIBAR ATEMBELEA VITENGO MBALIMBALI HOSPITAL YA MNAZI MMOJA

0
0
Mkuu wa wodi ya watoto Hospital ya Mnazi mmoja Fatma Ali Moh’d akimpatia maelezo Waziri wa Afya Hamad Rashid Mohamed mwenye Kaunda suti wakati Waziri huyo alipofanya ziara za Vitengo vya Hosptal hiyo.
Waziri wa Afya Zanzibar Hamad Rashid Mohamed akimjulia hali mtoto Khairat Juma anaesumbuliwa na ugonjwa wa kuvuja damu, kulia ni Mkuu ya wodi ya kina mama na watoto Hospital ya Mnazi mmoja Dkt. Nasra S Ali.
Mkurugenzi Mkuu Hospitali ya Mnazi mmoja Ali Salum Ali akielezea changamoto wanazokabiliana nazo katika utendaji wao wa kazi kwa uongozi wa Wizara ya Afya.
Mkuu ya Wodi ya kina mama na watoto Hospitali ya Mnazi mmoja Dkt. Nasra S Ali akielezea upungufu wa Wauguzi katika Wodi hiyo wakati uongozi wa Wizara ulipofanya ziara katia vitengo vya Mnazi mmoja.
Naibu Waziri wa Afya Zanzibar Harusi Said Suleiman akielezea maendeleo yaliyofikiwa licha ya changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika Hosptial ya Mnazi mmoja.
Waziri wa Afya Zanzibar Hamad Rashid Mohamed akizungumza na uongozi wa Wizara na Watendaji wa Hospital ya Mnazi mmoja mara baada ya kufanya ziara katika vitengo mbalimbali vya Hospital hiyo. Picha na Abdallah Omar-Maelezo Zanzibar

UBER IMEZINDUA HUDUMA MPYA YA uberPOA JIJINI DAR ES SALAAM

0
0
 
.Leo kampuni ya Uber imetangaza ujio wa huduma mpya ya uberPOA huduma hii ni ya bei nafuu inayolenga bajaji ikiwa ni juhudi za kupiga jeki huduma ya uberX jijini Dar es Salaam. Huduma hii mpya, ambayo wateja wataanza kufurahi kuanzia leo, itatolewa na bajaji au tukutuku ambazo zinatumia mafuta kidogo. uberPOA itawapa wasafiri wa sasa na wapya fursa ya kutumia huduma ya bei nafuu wanapofanya safari zao jijini Dar es Salaam.

Akizungumzia huduma hii, Meneja Msimamizi wa Uber nchini Tanzania, Bw. Alfred Msemo amesema, ‘Leo tunafuraha kubwa tunapozindua huduma hii ya uberPOA ambayo ni ya bei nafuu itakayotolewa na bajaji. Tuna furaha kwa sababu uberPOA inawapa wasafiri uhuru wa kuchagua huduma ya usafiri ambayo ni ya bei nafuu zaidi. Ujio wa huduma hii ni mkakati endelevu wa juhudi makusudi za kutumia ubunifu utakaoimarisha huduma tunazotoa katika kuafikia dhamira yetu ya kutoa usafiri salama, wa uhakika, na kwa bei nafuu jijini Dar es Salaam.”

uberPOA itatumia bajaji ambazo kwa ujumla hazina gharama kubwa ya matengenezo. Huduma ya UberPOA itatolewa sanjari na huduma ya sasa ya uberX inayotolewa na magari madogo ya aina ya sedan. “Tuna imani kwamba wasafiri jijini Dar es Salaam wana haki ya kuwa na uhuru wa usafiri ambao wangependa kutumia wanapofanya shughuli zao katika jiji letu, usafiri ambao ni wa bei nafuu na wenye kuleta ufanisi mkubwa katika maisha yao - uberPOA inatoa fursa hii.” Ameongeza Bw. Msemo.

Bei ya chini ya uberPOA itakuwa Tsh 1,500, Tsh 400 kwa kila KM, Tsh 80 kwa kila dakika, nei ya chini kabisa ambayo msafiri anaweza kulipa ni Tsh 2,000 na ada ya kughairi safari ni Tsh 2,000. “Kampuni ya Uber tunaamini ya kwamba wasafiri na washirika wetu wana kila sababu ya kujua nauli watakayolipa na namna wanavyotumia Uber katika shughuli zao za kila siku.” Amesema Bw. Msemo.

Wakati wa kuzindua huduma hii ya UberPOA, kampuni ya Uber imekariri kwamba imeweka mkakati utakaowahikikishia madereva kiasi fulani cha mapato katika kipindi hiki wanapozindua huduma hii hapa jijini. Ili wasafiri wapate huduma hii, wanatakiwa kufungua programu yao ya Uber ambapo watakuwa na nafasi ya kuita usafiri wa UberPOA au UberX. Kwa sasa huduma ya uberPOA inapatikana maeneo ya Mwenge, Sinza, Kijitonyama, Mikocheni A, Mwananyamala, Kinondoni, Namanga, Msasani, Oysterbay, Masaki & Kigamboni ingawa huduma hii inasambaa maeneo mengi katika siku za baadaye.

Uber imejijengea utaratibu wa kuzindua bidhaa mpya, hali ambayo inaleta upatikanaji wa huduma aina mbalimbali ambazo zitakuwa na tija kubwa kwa wasafiri na madereva washirika. Katika nchi jirani ya Kenya, tayari kampuni ya Uber imezindua huduma kadhaa kama vile uberCHAPCHAP, uberX na UberSELECT. Katika miji mbalimbali duniani kampuni ya Uber inatoa huduma kama vile uberMOTO, UberXL, UberBLACK, UberCHOPPER, UberASSIST, UberEXEC na UberPool.

TPDC YAIMARISHA SEKTA YA AFYA KIDUNDAI, LUSHOTO

0
0
Mwenyekiti wa Kijiji cha Kidundai, Ndg. Waziri Mdoe (Kushoto) akipokea mfano wa hundi ya shilingi milioni nne kutoka kwa mwakilishi wa TPDC, Ndg. Asiad Mrutu (Kulia). Makabidhiano hayo yalifanyika mbele ya jengo la zahanati inayoendelea kujengwa katika Kijiji hicho. 

 Katika jitihada endelevu za utekelezaji wa dhana ya uwajibikaji kwa jamii, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) ambalo ni Shirika la Mafuta la Taifa kwa mujibu wa Sheria ya Petroli (2015) limeendelea kuitekeleza dhana hiyo kwa vitendo kwa kutoa vifaa vya ujenzi wa Zahanati ya kijiji cha Kidunda Wilayani Lushoto Mkoani Tanga.

 Katika tukio hilo lililofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita, TPDC imeweza kukabidhi hundi ya Shilingi milioni nne ambazo Kijiji kiliomba kusaidiwa ili kuwezesha ujenzi wa zahanati hiyo ambapo kwa mujibu wa serikali ya Kijiji, fedha hizo zitawezesha manunuzi ya mizunguko ya nondo 40 yenye futi 40 kila moja, mifuko ya saruji, matofali na gharama za kumlipa fundi ambapo mpaka kufikia hapo zahanati itakuwa imefanikiwa kuezekwa. 

Akizungumza na mwandishi wa habari mara baada ya kumaliza makabidhiano, Mwenyekiti wa Kijiji cha Kidundai kilichopo Kata ya Vuga, Waziri Mdoe alisema “kwa niaba ya halmashauri ya kijiji, tunayo furaha isiyo kifani kwa ndugu zetu kutoka TPDC kwa moyo wa kutoa walioonyesha kwa kusaidia ujenzi wa zahanati yetu ambayo ilianza kujengwa kwa nguvu za wananchi wa kijiji hicho ili kuondokana na adh ya kutembea umbali wa kilomita nane ili kupata huduma ya afya”. 

Mdoe aliongezea kuwa, ni matumaini ya kijiji kwamba TPDC litaendelea kuwa mdau mkubwa wa maendeleo katika Kijiji cha Kidundai kwani mahitaji yao ni mengi yakiwemo maji, barabara na shule Akikabidhi mfano wa hundi kwa Mwenyekiti wa Kijiji kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Asiad Mrutu ambaye ni Mjiolojia alisema “kipekee nimshukuru Mwenyekiti na Wajumbe wa Serikali ya Kijiji kwa ushirikiano waliouonyesha toka tulipofika siku ya kwanza katika Kijiji hiki tukiwa na lengo la kutafuta eneo la uwekezaji, niseme tu kuwa huu ni mwanzo na tutaendelea kushirikiana bega kwa bega kusukuma gurudumu la maendeleo ya Kidundai mbele.” 

 Pamoja na kukabidhi hundi hiyo, Mrutu aliusisitiza uongozi wa Kijiji kuchanganua gharama za miradi ya maendeleo iliyopo katika mipango ili kurahisisha pale ambapo mdau wa maendeleo anaetaka kuchangia kufahamu ni kiasi gani kitatosha badala ya kueleza mahitaji kwa ujumla, hii itasaidia kupata msaada kirahisi na pia kupata msaada unaokidhi mahitaji ya mradi husika. 

Mchango wa ujenzi wa zahanati hiyo umekuja baada ya TPDC kufanikisha zoezi la kupata ardhi kwa ajili ya miradi ya kimkakati ya utafiti wa mafuta na gesi hapa nchini kwa lengo la kuongeza kiasi cha gesi asilia nchini ambacho kwa sasa ni futi za ujazo trilioni (TCF 57.538) na upatikanaji wa mafuta ili kuweza kulihakikishia taifa nishati ya kutosha kwa ajili uzalishaji wa umeme, vyombo vya usafiri, matumizi ya nyumba na kuhakikishia nishati ya kutosha kwa maendeleo ya viwanda nchini.

TAARIFA YA UFAFANUZI KUHUSU RAIA WA TANZANIA NCHINI OMAN

0
0



Kuna kipande cha video kinasambaa mitandaoni kikiwa na maelezo kuwa raia wa Tanzania wanaoishi nchini Oman wamekusanyika ofisi ya Ubalozi kushinikiza kurejeshwa nyumbani kutokana na mateso na adhabu kali wanazopata kutoka kwa mabosi wao.

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, baada ya kutazama kipande hicho cha video iliwasiliana na Ubalozi wa Tanzania nchini Oman kwa madhumuni ya kujua usahihi wa jambo hilo.

Ubalozi ulitoa ufafanuzi kuwa uliandaa mkutano wa Watanzania wote wanaoishi Oman na ulipangwa kufanyika katika hoteli ya Golden Tulip jijini Muscat tarehe 23 Machi 2018. Matangazo ya mkutano huo yalitaka Watanzania watakaopenda kushiriki wajisajili kabla ya siku ya mkutano. Watanzania takriban 200 walijisajili na ubalozi ulifanya maandalizi ya ukumbi, vyakula na vinywaji kwa ajili ya watu 300 kwenye hoteli ya Golden Tulip.

Siku ya mkutano ilipowadia, Watanzania zaidi ya elfu moja walijitokeza na kusababisha ugumu wa kuendelea na mkutano kutokana na maandalizi yaliyofanywa yalilenga watu 300. Kamati ya maandalizi ilipoona ukumbi umejaa na watu walio nje ni weng mara mbili zaidi ya watu waliokuwemo ndani ya ukumbi iliamua kufunga milango na kuwaomba waliochelewa warejee nyumbani.

Uamuzi huo haukuwafurahisha watu waliochelewa, hivyo walishinikiza waingizwe kwenye ukumbi wa mkutano, kitendo ambacho kiliashiria uwezekano wa kutokea vurugu kubwa.Kutokana na uhalisia huo, Kamati ya maandalizi ambayo ilijumuisha pia viongozi wa Watanzania wanaoishi nchini humo ilishauriana na kuamua kuwa mkutano huo uahirishwe na maandalizi yaanze upya kwa madhumuni ya kupata ukumbi na huduma nyingine zitakazokidhi idadi kubwa ya watu.

Kutokana na ufafanuzi huo, Wizara inapenda kuufahamisha umma wa Watanzania kuwa kipande hicho cha video kimechukuliwa wakati Watanzania wanashinikiza kuingia kwenye ukumbi wa mkutano na sio kwamba wamekusanyika kwenye ofisi ya ubalozi wa Tanzania kushinikiza kurejeshwa nyumbani kutokana na mateso wanayoyapata.


Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam, 26 Machi, 2018

Wawekezaji Wazawa Wapewa Rai Kujenga Viwanda vya Dawa

0
0
    

KAMATI YA BUNGE YA BAJETI YAENDELEA NA VIKAO VYAKE MJINI DODOMA

0
0
 Mwenyekiti wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Bajeti, Mhe. Hawa Ghasia akizungumza na Wajumbe wa kamati hiyo pamoja na viongozi wakuu kutoka Wizara ya fedha na Mipango walioongozwa na Waziri wa fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Mpango wakati wa kupitia na kujadili Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa fedha 2018/2019, katika kikao kilichofanyika leo ukumbi wa Pius Msekwa Mjini Dodoma.
Mjumbe wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Bajeti, Mhe. Albert Ntabaliba akizungumza wakati wa kupitia na kujadili Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa fedha 2018/2019 katika kikao kilichofanyika leo ukumbi wa Pius Msekwa Mjini Dodoma.

  Mwenyekiti wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Bajeti, Mhe. Hawa Ghasia akizungumza na Wajumbe wa kamati hiyo pamoja na viongozi wakuu kutoka Wizara ya fedha na Mipango (hawapo kwenye picha) wakati wa kupitia na kujadili Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa fedha 2018/2019. Kushoto ni Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Mpango katika kikao kilichofanyika leo ukumbi wa Pius Msekwa Mjini Dodoma.
Mjumbe wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Bajeti, Mhe. Maria kangoye akizungumza wakati wa kupitia na kujadili Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa fedha 2018/2019 katika kikao kilichofanyika leo ukumbi wa Pius Msekwa Mjini Dodoma. kushoto ni Mjumbe wa kamati hiyo Mhe. Riziki Lulidi
(PICHA NA OFISI YA BUNGE)

DC MATIRO APIGISHA KURA ZA SIRI KUBAINI WAUAJI WA WANAWAKE SHINYANGA VIJIJINI

0
0
Na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Kufuatia kuibuka kwa taarifa za kuwepo kwa mauaji ya wanawake yanayoambatana na imani za kishirikina katika kata ya Salawe wilaya ya Shinyanga, mkuu wa wilaya hiyo Josephine Matiro amefanya mkutano na wananchi wa eneo hilo kwa ajili ya kutafuta chanzo na ufumbuzi kumaliza mauaji hayo.

Wananchi wa kijiji cha Songambele kata ya Salawe wanasema mauaji hayo yameanza kutokea tangu mwezi Desemba mwaka jana wakidai kuwa wanawake hukatwa mapanga ama kunyongwa na watu wasiofahamika ambao hutoweka na viungo vya siri vya wanawake wanaowaua. 

Inaelezwa kuwa katika kipindi cha  Januari Mosi hadi Machi 23 mwaka huu watu waliouawa katika kata hiyo ni wanne huku mauaji hayo yakihusishwa na imani za kishirikina.Kutokana na hali hiyo Mkuu wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama wilaya hiyo, alifika katika kata ya Salawe kwa ajili ya kutafuta ufumbuzi wa mauaji hayo kwa njia ya kuwashirikisha wananchi.

Aidha baada ya kuzungumza na wananchi wa eneo hilo katika mkutano wa hadhara,mkuu huyo wa wilaya aliagiza kufanyika/kupigwa kwa kura za maoni kwa ajili ya kuwabaini wahusika wa mauaji hayo na kuondoka na kura hizo kwa ajili ya kuzifanyia kazi.

“Katika wilaya ya Shinyanga kuna kata 43, matukio ya mauaji ya namna hii yanatokea hapa,ni nyinyi hapa tu,sasa tumtafute mchawi na tumfanyie kazi,mkitaka kulimaliza tatizo hili ni  lazima mtupe ushirikiano,muwe tayari kufika mahakamani pale mtakapohitajika ,mjitokeze kutoa ushahidi ili wale watu msiwaone tena kwenye mitaa yenu”,alisema Matiro.

“Wananchi mmeendelea kulalamika kuwa kuna mauaji na kuitupia lawama serikali wakiwemo askari polisi kuwa wanapokea rushwa na kuwaachia huru watuhumiwa kumbe tatizo ni nyinyi kutotoa ushirikiano,naomba mbadilike, wafichueni wahusika ili tukomeshe tatizo hili kwani tunataka watu wawe salama na waishi kwa amani”,alieleza Matiro.

Aidha aliwataka viongozi wa serikali za mitaa na wananchi kwa ujumla kuacha kupokea wageni na kwamba wageni wote wajitambulishe ili kujua wanafanya nini na wametoka wapi ili kukomesha
Wakizungumza mbele ya mkuu wa wilaya ya Shinyanga, wananchi hao walisema matukio hayo yanatishia usalama wao na kusababisha waishi kwa hofu.

Walisema mbali na kuishi kwa hofu pia wanashindwa kufanya kazi zao za maendeleo na uzalishaji mali.Kwa mujibu wa Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga, ACP Simon Haule aliyekiri kuwepo kwa mauaji katika kata ya Salawe alisema chanzo ni kuwania mali,migogoro ya mashamba,wivu wa mapenzi na imani za kishirikina.

Aidha aliwataka wananchi kupuuza uzushi kwamba kwenye kata hiyo kuwa kuna watu wanakata mapanga wanawake na kisha kuondoka na sehemu zao nyeti yakiwemo matiti. 

“Kwenye mkoa wa Shinyanga hakuna kitu kama hicho, isipokuwa kuna takwimu za wananchi 27 kuuawa kwa kukatwa mapanga kutokana na sababu mbalimbali kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo kuanzia (2016- Machi 2018) ambapo wanawake 12, na wanaume 15. 

Alitaja takwimu za mauaji mkoa wa Shinyanga kwa kuchambua kila mwaka ambapo mwaka (2016) waliuawa watu 12, wanawake Sita, Wanaume Sita, (2017) wanaume nane, wanawake wanne, mwaka huu (2018) kuanzia Januari hadi Machi wanawake wawili na mwanaume mmoja jumla watu 27. 

Wananchi wakimsikiliza mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akiwasisitiza wananchi kutoa ushirikiano katika vyombo vya sheria ili kukomesha mauaji katika kata ya Salawe
Wananchi wakimsikiliza mkuu wa wilaya ya Shinyanga

Rais Magufuli azindua magari 181 ya Bohari kuu ya Madawa (MSD) jijini Dar es Salaam

0
0

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akikagua ghala ya dawa kwenye hafla ya uzinduzi wa magari 181 ya Bohari kuu ya Madawa (MSD) jijini Dar es salaam leo Machi 26, 2018. Pamoja naye ni Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu, Mwakilishi wa Taasisi ya Global Fund Bw. Linden Morrison na viongozi wengine.
 Sehemu ya  magari 181 ya Bohari kuu ya Madawa (MSD) yaliyozinduliwa  jijini Dar es salaam leo Machi 26, 2018.
  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akimshukuru  Mwakilishi wa Taasisi ya Global Fund, Bw. Linden Morrison wakati akijaribu moja ya magari 181 ya Bohari kuu ya Madawa (MSD) aliyozindua jijini Dar es salaam leo Machi 26, 2018.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akikagua sehemu ya magari  181 ya Bohari kuu ya Madawa (MSD)  aliyozindua jijini Dar es salaam leo Machi 26, 2018.Pamoja naye ni Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu, Mwakilishi wa Taasisi ya Global Fund, Bw. Linden Morrison na viongozi wengine.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akihutubia
kwenye hafla ya uzinduzi wa magari 181 ya Bohari kuu ya Madawa (MSD) jijini Dar es salaam leo Machi 26, 2018.
 Sehemu ya wafanyakazi wa MSD wakimshangilia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli  wakati akihutubia kwenye hafla ya uzinduzi wa magari 181 ya Bohari kuu ya Madawa (MSD) jijini Dar es salaam leo Machi 26, 2018.
  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akiongozana na Mwakilishi wa Taasisi ya Global Fund Bw. Linden Morrison wakati akijaribu moja ya magari  181 ya Bohari kuu ya Madawa (MSD) aliyozindua jijini Dar es salaam leo Machi 26, 2018.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akikata utepe
kwenye hafla ya uzinduzi wa magari 181 ya Bohari kuu ya Madawa (MSD) jijini Dar es salaam leo Machi 26, 2018. Pamoja naye ni Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu, Mwakilishi wa Taasisi ya Global Fund Bw. Linden Morrison na viongozi wengine.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akiwa na Mwakilishi wa Taasisi ya Global Fund Bw. Linden Morrison akijaribu moja ya magari  181 ya Bohari kuu ya Madawa (MSD) aliyozindua jijini Dar es salaam leo Machi 26, 2018.
 PALE WAPIGA PICHA WANAPOPIGWA PICHA - Wapiga picha wa vyombo mbalimbali vya habari wakiupiga picha msafara wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akiwa na Mwakilishi wa Taasisi ya Global Fund Bw. Linden Morrison  (chini kushoto) na viongozi wengine wakati wakielekea kukagua  magari  181 ya Bohari kuu ya Madawa (MSD) aliyozindua jijini Dar es salaam leo Machi 26, 2018.

Picha  na IKULU

MWALIM MKUU KAKONKO AJINYONGA AKIWA OFISINI KWAKE,AANDIKA UJUMBE MZITO

0
0

Na Rhoda Ezekiel, Kigoma

MKUU wa Shule ya Sekondari Kakonko wilayani Kakonko mkoani Kigoma,Peter Rubonya amefariki dunia baada ya kujinyonga kwa kamba ofisini kwake mapema leo asubuhi.

Akielezea tukio hilo,Mwalim wa zamu wa shule hiyo Isaac Japhet amesema yeye alifika shuleni hapo saa 12:30 asubuhi ili kuwafundisha wanafunzi wa kidato cha nne masomo ya ziada baada ya kufunga shule wiki iliyopita na baada ya kufika aligundua kuwa hana chaki ambapo mkuu huyo wa shule alimpatia chaki mlinzi ili awape wananfunzi.

Amesema baada ya muda,Mratibu elimu kata pamoja na mmoja wa wazazi walifika ofisini hapo wakiwa na shida na mkuu wa shule na baada ya kuelezwa yupo ndani ofisini lakini baada ya kugonga mlango hawakuweza kujibiwa na ndipo wakaamua kufungua mlango na kukuta mwili wa marehemu ukining’inia dalini.

Mwalim Isaac amesema Mwalimu aliyejinyonga alikuwa akifundisha masomo ya Kemia na Fizikia shuleni hapo hawakuwahi kusikia mgogoro wowote wa kifamilia au kijamii, na mkewe ambaye ni mkufunzi katika Chuo Kikuu cha Dodoma(UDOM),alifika nyumbani kwake juzi akitokea Dodoma.

Kwa upande wa Mlinzi wa Shule hiyo Kajolo Kajabojabo amesema alikutana na Mkuu wa shule mapema asubuhi akiingia ofisini na kumuomba chaki ambazo alipewa na kuziwasilisha kwa walimu."Nilimuona kabisa tukasalimiana, nikamuuliza kama anaweza kuwa na chaki, akaingia ofisini akanipatia boksi moja la chaki.Nikachukua na kisha nikampelekea mwalim aliyehizihitaji, alikuwa kwenye hali nzuri tu, lakini baada ya muda ndo tukio hilo likatokea,"amesema Kajoro.

Akizungumza baada ya kufika shuleni hapo Mkuu wa Wilaya ya Kakonko Kanali Hosea Ndagala amesema Polisi wanaendelea na uchunguzi wa tukio hilo kujua sababu ikiwa marehemu aliacha ujumbe wowote au laa.Hatujajua sababu lakini ni muhimu jamii ikajenga utamaduni wa kueleza matatizo ya ndani yanayoyasibu.Hiyo inasaidia kupunguza msongo wa mawazo na kuepusha madhara kama haya,"amesema.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma Martin Otieno amesema baada ya kupekuliwa kwa mwili wa marehemu walikuta karatasi imeandikwa ujumbe kuwa Mkurugenzi wa halmashauri ya Kakonko Lusubiro Mwakabibi asipodhibitiwa ataua wengi.

"TUNA WAJIBU WA KULINDA UTAMADUNI WA NCHI YETU"-WAZIRI MWAKYEMBE

0
0

MAVUNDE AIPONGEZA OSHA KWA KUBORESHA UTENDAJI WAKE

0
0
Wafanyakazi waliokingwa ipasavyo wakifanya kazi za ujenzi katika mradi wa reli ya kisasa kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro katika awamu ya kwanza ya mradi huo. OSHA huhakikisha kwamba wafanyakazi wanafanya kazi zao katika mazingira salama

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Mh. Antony Mavunde, ameupongeza Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) kwa jitihada unazozichukua katika kuimarisha hali ya usalama na afya katika sehemu za kazi nchini.

Mh. Mavunde alizitoa pongezi hizo alipozungumza na wafanyakazi wa OSHA katika kikao cha pili cha baraza la tatu la watumishi hao kilichofanyika jijini Arusha mwishoni mwa wiki.

“Niwapongezi kwa kazi nzuri mnayoifanya katika kuboresha hali ya usalama na afya katika maeneo ya kazi hapa nchini. Kwakweli kumekuwa na mabadiliko makubwa sana katika utendaji wenu hasa katika kipindi cha hivi karibuni,” alisema Mh. Mavunde.

Aliongeza: “Kipindi cha nyuma mlikuwa mnafanya kazi zenu kama askari polisi jambo ambalo lilikuwa linawapa hofu kubwa wadau wenu ambao badala ya kuuelewa wajibu wao kisheria na kuutekeleza, waliishia kuwakwepa na kuwalalamikia.”

Kiongozi huyo wa serikali alieleza kwamba kwasasa watumishi wa OSHA wamekuwa wakijitahidi kufanya kazi kwa weledi mkubwa ikiwemo kuwaelimisha wadau ili waweze kuutambua wajibu wao kisheria na kuutekeleza bila kushurutishwa.

Kwa upande wake Mgeni Rasmi katika kikao hicho ambaye pia ni Katibu Mkuu (Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu), Eric Shitindi, aliwataka watumishi wa OSHA kuendelea kutekeleza majukumu yao katika namna ambayo itaboresha zaidi huduma kwa wanufaika wake.

“Kipindi cha nyuma kulikuwa na malalamiko mengi sana kutoka kwa watu tunaowahudumia lakini kwasasa malalamiko yamepungua sana. Hivyo nawaomba muendelee kutoa huduma nzuri kwa wateja wenu kwa kuzingia vyema Sheria na Kanuni mbali mbali zilizopo,” alisema mgeni rasmi.

Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala, Khadija Mwenda, alisema kikao hicho cha baraza la wafanyakazi kinalenga kufanya tathmini ya utendaji wa taasisi kwa kipindi kilichopita na kuweka mikakati ya kujiimarisha zaidi kiutendaji kwa kipindi kijacho.

Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) ni taasisi ya serikali yenye dhamana ya kusimamia masuala ya Usalama na Afya za wafanyakazi wanapokuwa katika sehemu zao za kazi. Wakala hufanya kaguzi za kiusalama na afya katika sehemu zote za kazi hapa nchini. OSHA pia huwashauri wamiliki ama wasimamizi wa maeneo ya kazi juu ya uwekaji na usimamizi wa mifumo ya kulinda afya na usalama wa wafanyakazi wanapokuwa kazini.

Taarifa kutoka kwa Waziri Mwakyembe kuhusu Maudhui ya Mtandaoni.

0
0











EFM YAWEKA MILIONI 300 SHINDANO LA SHIKA NDINGA

0
0
Na Humphrey Shao, Globu ya Jamii
Mkurugenzi Mkuu wa kituo cha Efm Radio, Dennis Busulwa(SEBO) amesema kampuni yake imewekeza kiasi cha zaidi Milioni 300 kwa ajili ya shindano lake la Shika Ndinga  litakalofanyika katika mikoa 6 ya Tanzania bara  na kuanza kutimua vumbi Dar es Salaam katika uwanja wa Mwembe Yanga.

Sebo amesema hayo jijini Dar es Salaam leo alipokuwa anazungumza na Waandishi wa habari juu ya uzinduzi wa shindano hilo na maadhimisho ya miaka minne ya Efm Radio na kuongezeka kwa masafa kwa kutoka mikoa sita hadi kufika kumi.

"Efm Radio imekuwa na bidhaa mbalimbali za uwezeshaji  kwa wasikilizaji wake ambapo shika ndinga kwa mwaka huu 2018 linaweza kuwafikia watanzania katika mikoa sita zaidi ikiwa ni lengo la uwezeshaji katika jamii "amesema Sebo.

Amesema Shindano la shika ndinga mwaka huu linatarajia kufanyika kwa wiki 7 katika mikoa sita amabayo ni Dar es Salaam, Tanga, Mwanza, Mtwara , Mbeya na Pwani  ambapo litaanza tarehe 7 April hadi mei 15 ikihusisha jumala ya Pikipiki 14 na gari aina ya kirikuu mbili.

katika hatua nyingine Sebo alitumia mkutano kuwaeleza waandishi wa habari juu ya mafanikio ya Radio yao katika miaka minne tangu kuanzishwa kwake  kwa kuwa radio namba moja kwa kusikilizwa kwa mikoa ya Dar es Salaam na Pwani huku ikiwa namba mbili katika mikoa ya bara.
 Afisa Habari wa Kampuni ya Michezo ya Kubahatisha ya Tatu Mzuka ,Petronila Mtatiro akieleza namana watu watakavyoweza kujishindia zawadi mbalimbali wakati wa shindano la shika ndinga.
 Meneja Mkuu wa EFM Radio,Dennis Busulwa(SEBO), Akizungumza na Waandishi wa Habari Jijini Dar es Salaam leo juu ya shamrashamra za Efm Kutimiza miaka minne sanjari na uzinduzi wa Shindano la Shika ndinga linaloendeshwa na kituo hicho cha Radio kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.
 Afisa Uhusiano wa Shirika la Simu nchini(TTCL), Nicodemus Mushi akizungumza na Waandishi wa habari juu ya udhamini wa shirika lake katika mashindano ya shika ndinga kote nchini.
 Mkurugenzi wa kampuni ya Chotec Limited inayosambaza vilainishi vya Shell, Tanzania, Choba Mumba akieleza namna wao watakavyoweza kusambaza vilainishi maalum vya pikipiki nchini.
 Meneja Matukio wa Kampuni ya Efm Radio, Jesca Mwanyika akizungumza juu ya matokeo ya washindi wa shindano la Shika ndinga katika msimu uliopita .
 Baadhi ya Wadau na wadhamini wakifatilia mkutano wa Waandishi wa habari juu ya shindano la Shika Ndinga na Miaka Minne ya Efm.
Sehemu ya Waandishi wa Habari wa waliohiriki Mkutano juu ya shindano la shika ndinga na Miaka minne ya Efm.

WAHAMIAJI HARAMU WAKAMATWA PINGO/MKOANI PWANI-RPC SHANNA

0
0


Wahamiaji haramu kutoka nchini Ethiopia ambao wamekamatwa na jeshi la polisi Mkoani Pwani ,huko porini Pingo shule ,wilaya ya kipolisi Chalinze.
 Kamanda wa polisi Mkoani Pwani, (ACP) Jonathan Shanna akizungumza kuhusiana na misako na doria zinazoendelea Mkoani humo.
 Kamanda wa polisi Mkoani Pwani, (ACP) Jonathan Shanna akiakionesha baadhi ya siraha alizokamata.

Na Mwamvua Mwinyi,Pwani
JESHI la polisi mkoani Pwani, limewakamata wahamiaji haramu kumi raia wa nchi ya  Ethiopia ,kwa kosa la kuingia nchini bila kibali.

Jeshi hilo pia, limemtia nguvuni mwanamke -Siwema Mgombale akiwa na risasi 23 zinazotumika kwenye silaha aina ya shortgun, huko kijiji cha Manda Mazingara kata ya Miono,tarafa ya Mkange wilaya ya Bagamoyo.

Kamanda wa polisi mkoani Pwani, (ACP), Jonathan Shanna alisema, wahamiaji haramu hao wamekamatwa machi 26, wakiwa porini ,Pingo Shule ,wilaya ya kipolisi Chalinze na askari waliokuwa doria kufuatia kupata taarifa kutoka kwa raia wema.

Akielezea matukio mbalimbali yaliyotokea mkoani hapo, aliwataja waliokamatwa kuwa ni Tagen Alam (19), Abraham Wolde (19) na Musama Kamal (16).

Wengine ni Abush Tamaskel (16), Ayela Erapo (18) na Ngusie Kechine (18), Zarabel Faisa (16), Tsedhj Yshgee (19), Teyey Ally (18) na Tuktigo Clemag (17).

Watuhumiwa wote hao watafikishwa idara ya uhamiaji kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria.

Kamanda Shanna alielezea ,jeshi hilo linaendelea na juhudi za kuwatafuta watu waliowasaidia kuingia nchini bila kufuata utaratibu wa sheria.

Katika tukio jingine , mwanamke aliyejulikana kwa jina la Felister Mtinga (30-36) amekutwa kitandani akiwa amefariki dunia katika nyumba ya kulala wageni iitwayo Moreto,iliyopo Chalinze.

Kamanda Shanna alisema kuwa, mwili wa mwanamke huyo ulibainika machi 26 mwaka huu majira ya saa nne asubuhi baada ya wahudumu kutomuona akitoka tangu alipoingia ndani machi 25 katika nyumba hiyo.

Alifafanua , mwili wa marehemu umeshafanyiwa uchunguzi wa awali na kubaini kutokuwa na majeraha ya aina yoyote hali inayosababisha kuondoa mashaka kuhusu kifo chake na umehifadhiwa katika hospitali ya Rufaa ya mkoa ya Tumbi.

Katika tukio la kukutwa na silaha, kamanda Shanna alibainisha wamekamata silaha mbalimbali katika misako inayoendelea kufanyika mkoani hapo, ikiwemo SMG .R.6134, mapanga manne, sime moja na risasi 23.

Alieleza, saa sita usiku machi 27,walimkamata mwamke aliyetambulika kwa jina la Siwema Mgombale akiwa na risasi 23 zinazotumika kwenye short gun na Ramadhani Mdoe akiwa na silaha aina ya SMG.R.6134 .

“Tunaendelea na misako kabambe inayoongozwa na kikosi chao cha siri, tunafanya misako uvungu kwa uvungu,giza kwa giza,pori kwa pori,tunashukuru inazidi kufanikiwa na ni endelevu “alisisitiza kamanda huyo.

Kamanda Shanna aliwaomba wananchi kushirikiana na jeshi la polisi kutoa taarifa za wale wachache ambao wanawadhania ni wahalifu kwenye maeneo yao.

RAIS MHE. DKT. MAGUFULI APOKEA RIPOTI YA MDHIBITI NA MKAGUZI MKUU WA HESABU ZA SERIKALI CAG KWA MWAKA WA FEDHA UNAOISHIA TAREHE 30 JUNE 2017

0
0


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa  Dkt. John Pombe Magufuli akipokea Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Profesa Mussa Assad Ikulu jijini Dar es Salaam.
4
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa  Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) mezani kwake mara baada ya kuzipokea kutoka kwa CAG Profesa Mussa Assad Ikulu jijini Dar es Salaam.
5.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa  Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza wakati akitolea ufafanuzi baadhi ya hoja  zilizowasilishwa katika taarifa hiyo ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Profesa Mussa Assad Ikulu jijini Dar es Salaam.
7
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa  Dkt. John Pombe Magufuli akipiga makofi wakati viongozi wa Kamati mbalimbali za  Bunge walipokuwa wakizungumza mara baada ya uwasilishwaji wa taarifa hiyo ya CAG
11
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa  Dkt. John Pombe Magufuli akimkabidhi Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa ajili ya kwenda kuifanyia kazi pamoja na Mawaziri, Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu na Wakuu wa Taasisi mbalimbali za Serikali.
13
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa  Dkt. John Pombe Magufuli akimpongeza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Profesa Mussa Assad mara baada ya kupokea Ripoti yake Ikulu jijini Dar es Salaam. Katikati ni Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.
15
Baadhi ya Mawaziri waliohudhuri katika tukio la uwasilishwaji wa Taarifa ya Mdhibiti na  Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG wakifatilia kwa makini taarifa hiyo Ikulu jijini Dar es Salaam.
18
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa  Dkt. John Pombe Magufuli akiagana na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa mara baada ya kupokea Taarifa ya Mdhibiti na  Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG Ikulu jijini Dar es Salaam.
19
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa  Dkt. John Pombe Magufuli akiwa katika picha ya pamoja na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Profesa Mussa Assad pamoja na wafayakazi mbalimbali kutoka katika Ofisi yake mara baada ya kuwasilisha taarifa hiyo ya ukaguzi wa hesabu za Serikali kwa mwaka unaoishia tarehe 30 Juni 2017, Ikulu jijini Dar es Salaam.
PICHA NA IKULU


KIWANDA CHA GRANDE DEMAM CHAONGEZA THAMANI YA MAZIWA WILAYA YA ARUMERU

0
0
Na Woinde Shizza ,Arusha

WAKURUGENZI wa Kiwanda cha Grande Demam kilichopo wilayani Meru mkoani Arushawameama kuongeza thamani ya maziwa ya ng'ombe huku 
wakihamasisha Watanzania kunywa maziwa yalisindikwa kwani hayana madhara kwa mlaji zaidi ya kumkinga na magonjwa yanayoweza kuambikizwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu.

Uamuzi wa kuongeza thamani ya maziwa umetokana kiwanda hicho kuongeza wigo na kununua maziwa zaidi kwa wafugaji wilayani hapo ambao walikua wakiteseka kupata masoko na wakati mwingine kumwaga maziwa yao yanayoharibika kwa kukaa muda mrefu bila kununuliwa.

Imefahamika Wilaya ya Meru ni moja kati ya Wilaya maarufu zinazoongoza kwa uzalishaji mkubwa wa maziwa mkoani Arusha na maziwa hayo huuzwa maeneo ya miji ikiwemo viunga vya Jiji la Arusha na nje ya Jiji hilo.

Licha ya uzalishaji huo wa maziwa bado wafugaji hao wa wilaya hiyo ya Arumeru walikuwa wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa masoko ya uhakika ya kununua maziwa hayo, hivyo kusababisha kuharibika baada ya kukaa kwa muda mrefu bila kununuliwa.

Akizungumza leo mmoja wa wakurugenzi wa kiwanda hicho Dk.Deo ambaye ni mtaalam wa mifugo anasema kutokana na changamoto hiyo kwao wakaifanya kuwa fursa ya wao kuwekeza kiwanda cha kusindika maziwa.

Dk.Deo anasema kwa kuwa wafugaji hao walikua wakiyamwaga maziwa yao yaliyokuwa yakiharibika kwa kukosa soko la uhakika na hawakuwa na namna yoyote ya kuongeza thamani maziwa hayo ili yaweze kukaa kwa muda bila kuharibika baada ya kuanzisha kiwanda hicho imesaidia kuongeza thamani ya maziwa.

Anafafanua aliamua kuacha kazi mwaka 2001 na kuamua kufuga ng'ombe mmoja na baadae wakaongezeka kuwa wawili ambao walikuwa wanatoa lita 40 kila siku huku yeye na familia yake wakitumia lita moja,hivyo maziwa mengine yalikuwa yanaharibika.

"Hali hiyo ilinafanya nimtafute mtaalam kutoka Kenya ambaye atafundisha jinsi ya kuongeza thamani ya maziwa ya ng'ombe kwa kuyafungasha na kuyauza. Mtaalamu huyo alinifundisha na ndipo nilipoanza kuongeza thamani ya maziwa.

"Baada ya muda ya muda majirani zangu ambao ni wafugaji walianza kuvutiwa na jinsi ninavyoongeza thamani ya maziwa yake.Hivyo nao wakaanza kunufaika kwani nilianza kwa kununua lita 100, baadae nikawa nanunua lita 150 na sasa nanunua lita 200 kwa siku,"amesema Dk.Deo.
Anasema baada ya hapo akafungua kiwanda kidogo ambacho kilikua na uwezo wa kusindika lita 200 kwa siku huku wafugaji wakimpelekea maziwa zaidi ya hapo ndipo alipoongeza uzalishaji na sasa kwa siku anazalisha lita 2000.

Dk.Deo anasema kutokana na ongezeko hilo la uzalishaji ,wakurugenzi wenzake wa kiwanda hicho cha The Grande Demam wameongeza wigo na kununua maziwa zaidi kwa wafugaji ambao walikua wakiteseka kupata 
masoko na wakati mwingine kumwaga maziwa yao yanayoharibika.

Amefafanua kiwanda hicho kinanunua maziwa bora kutoka kwa wafugaji na kuyaongezea thamani ikiwa ni pamoja na kuyafungasha vyema.
"Maziwa ambayo hayajaongezwa thamani hukaa kwa muda wa saa 13 lakini maziwa yaliyoongezwa thamani yanakaa hadi mwezi mmoja jambo linalota unafuu hasa kwa kipindi kifupi kabla hayajafika sokoni".

Dk.Deo anaeleza maziwa yaliyosindwa ni mazuri kwa afya ya binadamu kwani yanakuwa yameondolewa bakteria na kuongezewa bakteria rafiki kwa afya.Mtu anayetumia maziwa yasiyosindikwa anakuwa na hatari ya kupata magonjwa mbalimbali ikiwemo TB, yphoid na Brusela.

Dk.Deo anasema maziwa ni bidhaa yenye faida kubwa katika mwili wa binadamu ikiwemo virutubisho aina ya protini,madini,fat na wanga na kufafanua unywaji wa maziwa uhamasishwe kwa wingi katika jamii ili kuwa na jamii yenye afya bora inayoweza kushiriki shughuli za uzalishaji.

"Tuna mpango wa kuzalisha mpaka lita 100,000 kwa siku na uzalishaji huu
utaleta tija kwa kiwanda na wafugaji ambao tumekua tukinunua maziwa 
kwao.Tutanunua maziwa mengi zaidi na hivyo tutaongeza kipato cha mfugaji ambao watanufaika na shughuli zao,"amesema Dk.Deo.

Amesema ni vema Watanzania wakajifunza kunywa maziwa haya bora yanayozalishwa nchini badala ya kunywa maziwa kutoka nje kwani kwa kufanya hivyo utakua unainua uchumi wa nje.

Dk.Deo amesema biashara ya maziwa imesaidia vijana wengi waliojiriwa na kiwanda hicho katika sekta ya uzalishaji na usambazaji jambo ambalo linaonesha mnyororo wa wanufaika wa kiwanda hicho unavyoongezeka."Kwa sasa bidhaa za maziwa,Yogat na Siagi za The Grande Demam imefika katika mikoa ya Dar es Salaam ,Manyara ,Tanga na Morogoro,"amesisitiza.

Kwa upande wa Mshauri wa Masuala ya Biashara katika kiwanda hicho Peter Ojukwu amesema kiwanda kimesaidia kunufaisha wananchi zaidi ya 4500 kutokana na mzunguko wa uzalishaji mpaka kumfikia mlaji.

"Licha ya kiwanda hicho kujikita na uzalishaji wa maziwa bado tunatoa huduma za ushauri wa ufugaji bora,matibabu ya mifugo na dawa ili waweze kufanya ufugaji wenye tija,"amesema.

Baadhi ya Wafanyakazi na Viongozi wa Kiwanda cha Maziwa cha The Grande Demam wakihakiki ufungashaji wa bidhaa za maziwa zinazozalishwa kiwandani hapo
Baadhi ya Viongozi wa kiwanda cha maziwa cha The Grande Demam wakinywa maziwa yanayozalishwa na kiwanda hichoBaadhi ya Viongozi wa kiwanda cha maziwa cha The Grande Demam wakinywa maziwa yanayozalishwa na kiwanda hicho


Uongozi wa kiwanda cha maziwa cha The Grande Demam 

MAKAMU WA RAIS, SAMIA SULUHU AFUNGUA MKUTANO WA SHIMMUTA

0
0
MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan amewataka Viongozi wa Mashirika ya Umma na Makampuni Binafsi kuwaruhusu wafanyakazi kushiriki michezo katika maeneo yao ya kazi lakini pia wawaruhusu wafanyakazi hao kushiriki Michezo ya SHIMMUTA.

Makamu wa Rais ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Halmashauri Kuu ya Shirikisho la Michezo la Mashirika ya Umma na Makampuni Binafsi Tanzania (SHIMMUTA) mjini Dodoma.

Makamu wa Rais amesema michezo ni muhimu sana kwenye Tanzania ya Viwanda kwani michezo husaidia mwili kuwa wenye afya bora na utendaji wao wa kazi unakuwa mzuri zaidi.
Makamu wa Rais amesema yeye alikuwa mwanamichezo mzuri wa mpira wa pete (netball) lakini kwa sasa anafanya mazoezi kidogo kidogo asubuhi na jioni.

“Najua Umuhimu wa kufanya mazoezi kwa sababu nikiacha kufanya mazoezi nadorora na katika nafasi hii ukidorora unadorora mpaka akili na kazi zitakushinda”

Makamu wa Rais aliwasihi Viongozi wa Michezo kusimamia masuala ya michezo katika maeneo ya kazi na kuwataka Viongozi wa Taasisi kuweka bajeti ya michezo kwa ajili ya kushiriki michezo ya SHIMMUTA.

Makamu wa Rais amesema ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya 2015- 2020 imeleekeza kuendeleza michezo sehemu za kazi.

Aidha Mwenyekiti wa SHIMMUTA Ndugu Hamis Mkanachi alimpongeza Makamu wa Rais kwa juhudi anazozifanya katika kukuza michezo nchini.

WAWEKEZAJI WAHIMIZWA KUJENGA VIWANDA VYA KUBANGUA KOROSHO NA KUTENGENEZA MAGUNIA -RC PWANI

0
0

Na Mwamvua Mwinyi,Pwani 

MKUU wa mkoa wa Pwani,mhandisi Evarist Ndikilo, amewahimiza wawekezaji wenye uwezo wa kujenga viwanda vya kubangua korosho na kutengeneza magunia ,kujenga viwanda hivyo ili kuwarahisishia wakulima wa zao hilo . 

Aidha amewaasa maafisa ugani mkoani hapo, kuacha kujibweteka maofisini kupigwa viyoyozi na badala yake watoke na kwenda kwa wakulima kutoa elimu mbalimbali za kilimo cha kisasa na chenye tija cha zao hilo. 

Alkadhalika, Ndikilo amewataka wakulima wa zao la korosho kufufua mashamba ya korosho pamoja na kupanda miche mipya ya mikorosho ili kuinua zao hilo kimkoa. 

Akizindua upandaji wa miche mipya ya mikorosho Ruvu JKT ,Vikuruti wilayani Kibaha Vijiji, alieleza msimu uliopita ulikumbwa na changamoto ya upungufu wa magunia hivyo kuna kila sababu ya kujengwa viwanda hivyo ili mkulima aweze kuwa na uhakika wa kupata magunia. 

Mkuu huyo wa mkoa alisema, miaka ya 60/70 mkoa wa Pwani ulikuwa ukizalisha kwa wingi lakini kwasasa mashamba mengi yametelekezwa hivyo kusababisha kushuka kwa kilimo hicho . 

“Baadhi ya wakulima walishindwa kupalilia,kuweka dawa na mashamba mengi yalitelekezwa, kutokana na hilo nachukua fursa hii kutoa rai kwa maafisa ugani, mtoke maofisini, mkawaelimishe wakulima wetu kuhusiana na kilimo chenye tija,na muwahimize wapande miche mipya” 

“Tumeamua kufanya uzinduzi huu ili kuonyesha umuhimu wa zao hili kimkoa na kitaifa kama mjuavyo serikali yetu ya awamu ya tano imeliingiza zao hili kuwa moja ya mazao ya kimkakati ikiwemo pamba, kahawa ,tumbaku na chai”, Katika kipindi hiki cha kujenga uchumi wa kati na viwanda ili kuinua pato la Taifa “alifafanua Ndikilo. 

Hata hivyo ,Ndikilo aliwataka viongozi wa vitongoji na vijiji kuanzisha madaftari ya wakulima kwa lengo la kupata takwimu zao na kuwafuatilia katika mipango mbalimbali ya masuala ya kilimo. 

Awali afisa kilimo wa mkoa wa Pwani, Specioza Kashangaki alieleza , kutokana na umuhimu wa zao la korosho, serikali kupitia bodi ya korosho Tanzania imesambaza mbegu bora ili miche itakayopatikana isambazwe bure kwa wakulima. 

Alisema kupitia utaratibu huo mkoa huo ulipokea kilo 7,182 zinazokadiriwa kutoa miche milioni.1.039,687 ambazo inatarajiwa kupandwa kote mkoani kipindi cha mvua za masika. 

Specioza alitaja changamoto zinazowakabili kuwa ni kutokuwepo na kumbukumbu sahihi za miche mipya inayopandwa kuanzia ngazi ya kijiji hadi mkoa na kutokuwepo kwa maghala bora ya kuhifadhia korosho hali inayoathiri ubora wa korosho. 

“Anabainisha”Kumekuwepo na udanganyifu mkubwa unaofanyika katika maghala ya kuhifadhia korosho ambapo baadhi ya AMCOS zimebainika kusabababisha uzito wakati wa mazao kutofautiana na uzito wa korosho wakati mnunuzi anakabidhiwa korosho zake. 

Akitoa taarifa ya uendelezaji wa zao hilo,katika shamba la Ruvu JKT ,meneja wa shamba , Godfrey Mwakabole alisema kitaalamu mikorosho inatakiwa kupandwa kwa nafasi mita 12 kwa mita 12, na kupata miche 28-30 kwa hekari moja. 

Kwa mujibu wa Mwakabole alisema, wamepanda miche mipya katika hekari 50 ambapo wamechanganya na zao la mahindi na shamba jingine la hekari 50 wamepanda miche hiyo na wanakaribia kuanza palizi. 

Miche ya mikorosho inatakiwa kutunzwa kwa kupaliliwa, kutengenezewa visahani, kupogolea,kudhibiti magonjwa na wadudu ambapo inashauriwa mikorosho ikiwa midogo kuchanganya mazao ya muda mfupi ili wakulima wapate mazao na kipato kwenye eneo moja.
Mkuu wa Mkoa wa Pwani ,Mhandisi Evarist Ndikilo ,akipanda mche mpya wa zao la mkorosho ,wakati wa uzinduzi wa upandaji wa miche mipya ya mikorosho Mkoani hapo ,uliofanyika ,Ruvu Jkt,huko Vikuruti Kibaha Vijijini. 
Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo ,alhaj Majid Mwanga ,akipanda mche mpya wa zao la mkorosho ,wakati wa uzinduzi wa upandaji wa miche mipya ya mikorosho Mkoani hapo ,uliofanyika ,Ruvu Jkt,huko Vikuruti Kibaha Vijijini. Picha na Mwamvua Mwinyi

AIRTEL YAFUNGUA OFISI WILAYA YA GAIRO

0
0
 Picha ya Pamoja mara baada ya kuzindua duka Wilayani Gairo.
Mkuu wa Wilaya ya Gairo Mhe. Siriel Shaidi Mchembe(Kulia) akilishwa keki wakati wa uzinduzi wa Ofisi ya Airtel Wilayani Gairo.

HATIMAYE Kampuni ya Simu ya Airtel yawatendea haki wana Gairo.
Hayo yamesemwa leo na Mkuu wa Wilaya ya Gairo Mhe. Siriel Shaidi Mchembe wakati wa uzinduzi wa Ofisi ya Airtel.

Kwa kiasi kikubwa mtandao wa Airtel ndio mkombozi mkubwa wa wananchi wa Gairo hasa vijijini. Bado mawasiliano  ya simu ni changamoto kubwa sana Gairo.

Mhe. Mchembe aliendelea kuwapongeza Airtel kwa ajira zaidi ya 400 nchini kupitia ofisi zinazozinduliwa sasa. Vijana wa Gairo pia ni wafaidika wa Ofisi hizo.

Kabla ya kufunguliwa ofisi hizo, wananchi walikuwa wanaenda Dodoma au Morogoro kwa huduma mbalimbali zinazohitaji kushughulikiwa na Airtel wenyewe.

Mhe. Mchembe anayakaribisha mashirika mengine ya simu kufungua ofisi Gairo. Wilaya inakuwa kwa kasi kubwa na mzunguko wa pesa ni mkubwa na mawasiliano yanahitajika kwa kasi kubwa.

EFM YAWEKA MILIONI 300 SHINDANO LA SHIKA NDINGA

0
0
--
Na Humphrey Shao, Globu ya Jamii

Mkurugenzi Mkuu wa kituo cha Efm Radio, Dennis Busulwa(SEBO) amesema kampuni yake imewekeza kiasi cha zaidi Milioni 300 kwa ajili ya shindano lake la Shika Ndinga  litakalofanyika katika mikoa 6 ya Tanzania bara  na kuanza kutimua vumbi Dar es Salaam katika uwanja wa Mwembe Yanga.

Sebo amesema hayo jijini Dar es Salaam leo alipokuwa anazungumza na Waandishi wa habari juu ya uzinduzi wa shindano hilo na maadhimisho ya miaka minne ya Efm Radio na kuongezeka kwa masafa kwa kutoka mikoa sita hadi kufika kumi.

"Efm Radio imekuwa na bidhaa mbalimbali za uwezeshaji  kwa wasikilizaji wake ambapo shika ndinga kwa mwaka huu 2018 linaweza kuwafikia watanzania katika mikoa sita zaidi ikiwa ni lengo la uwezeshaji katika jamii "amesema Sebo.

Amesema Shindano la shika ndinga mwaka huu linatarajia kufanyika kwa wiki 7 katika mikoa sita amabayo ni Dar es Salaam, Tanga, Mwanza, Mtwara , Mbeya na Pwani  ambapo litaanza tarehe 7 April hadi mei 15 ikihusisha jumala ya Pikipiki 14 na gari aina ya kirikuu mbili.

katika hatua nyingine Sebo alitumia mkutano kuwaeleza waandishi wa habari juu ya mafanikio ya Radio yao katika miaka minne tangu kuanzishwa kwake  kwa kuwa radio namba moja kwa kusikilizwa kwa mikoa ya Dar es Salaam na Pwani huku ikiwa namba mbili katika mikoa ya bara.
 Meneja Mkuu wa EFM Radio,Dennis Busulwa(SEBO), Akizungumza na Waandishi wa Habari Jijini Dar es Salaam leo juu ya shamrashamra za Efm Kutimiza miaka minne sanjari na uzinduzi wa Shindano la Shika ndinga linaloendeshwa na kituo hicho cha Radio kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.
 Afisa Uhusiano wa Shirika la Simu nchini(TTCL), Nicodemus Mushi akizungumza na Waandishi wa habari juu ya udhamini wa shirika lake katika mashindano ya shika ndinga kote nchini.
 Afisa Habari wa Kampuni ya Michezo ya Kubahatisha ya Tatu Mzuka ,Petronila Mtatiro akieleza namana watu watakavyoweza kujishindia zawadi mbalimbali wakati wa shindano la shika ndinga.
 Mkurugenzi wa kampuni ya Chotec Limited inayosambaza vilainishi vya Shell, Tanzania, Choba Mumba akieleza namna wao watakavyoweza kusambaza vilainishi maalum vya pikipiki nchini.
 Meneja Matukio wa Kampuni ya Efm Radio, Jesca Mwanyika akizungumza juu ya matokeo ya washindi wa shindano la Shika ndinga katika msimu uliopita .
 Baadhi ya Wadau na wadhamini wakifatilia mkutano wa Waandishi wa habari juu ya shindano la Shika Ndinga na Miaka Minne ya Efm.
Sehemu ya Waandishi wa Habari wa waliohiriki Mkutano juu ya shindano la shika ndinga na Miaka minne ya Efm.
Viewing all 46202 articles
Browse latest View live


Latest Images