|
Ndugu Abdulrahamani A.Alli Mwenyekiti Jumuiya ya Watanzania Italia |
Ndugu zangu,
Watanzania Wenzangu hapa Italia,
Nina furaha na faraja kubwa kuukaribisha mwaka 2013.
Ni jambo la bahati ambayo hatuna budi kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma, kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha kuumaliza mwaka wa 2012 salama.
Wapo ndugu, jamaa na marafiki zetu wengi ambao wangependa kuuona mwaka huu lakini hawakujaaliwa. Wametangulia mbele ya haki. kama mnavyojua tumekwisha safirisha miili ya Watanzania wenzetu watatu na mwili mmoja bado tupo katika hatua za mwisho ili tuweze kuusafirisha.
Tuendelee kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu awape mapumziko mema. Nasi tumuombe Mola wetu atujaalie baraka katika mwaka huu mpya 2013. AMIN!
Mwaka tulioumaliza ulikuwa wenye mambo mengi mazuri na mafanikio, lakini, pia, bado ulikuwa na changamoto zake. Baadhi zilikuwa ngumu na zipo zilizokuwa za kusikitisha na kuhuzunisha hasa za misiba.
Napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru wote kwa ushirikiano wenu kwa kujitolea kwa hali na mali katika kutatua matatizo makubwa yanayotufika hasa ya misiba. Nawashukuru viongozi na Watanzania wote wa matawi ya jumuiya yetu na jumuiya zingine za Watanzania hapa Italia. Kwa kweli mnastahili pongezi kubwa.Napenda kusisitiza umoja,ushirikiano na upendo baina yetu.
Nachukua nafasi hii pia kumshukuru Mh. Alex James Msekela Balozi wa Tanzania Rome Italy, na maofisa na watendaji wote wa Ubalozi wetu kwa ushirikiano wao wakati wote tunapowahitaji,kwenye furaha,matatizo mbalimbali.
Mafanikio:
Katika mwaka uliopita 2012 Jumuiya yetu kama nilivyosema mwanzo kuwa tulipata mafanikio na matatizo pia ambayo zaidi ilikuwa ni ya misiba na kuuguliwa.
Mafanikio tuliyoyapata ni kama ifuatavyo:
- Kwanza kabisa katika mwaka wa 2012 idadi ya Wanajumuiya imeongezeka zaidi, hii inaonyesha jinsi gani Watanzania wanavyoridhika na utendaji mbalimbali wa Jumuiya yetu.
- Vilevile kwa mwaka wa 2012 Jumuiya yetu ilishiriki mikutano kadhaa ya jumuiya zingine na kupata mialiko mbalimbali ya kuhudhuria sherehe za kitaifa pamoja na ufunguzi wa jumuiya mpya za mataifa mengine.Hili limetuongezea zaidi uzoefu na kujifunza mengi kutoka kwa wenzetu.
- Mwaka 2012 tulipata heshima kubwa ya kushiriki mapokezi ya ugeni mkubwa wa serikali yetu ulioongozwa na spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Anne Makinda ,kwa ajili ya mkutano wa mzingira wa kimataifa uliofanyika mjini Napoli, Katika mkutano huo ambao pia ulihudhuriwa na balozi wa Tanzania Rome, Mh Alex James Msekela, mheshimiwa balozi alipata fursa ya kuongea na Watanzania na kujitambulisha rasmi kuwa Balozi mpya wa Tanzania baada ya M h. Ali Karume.
- Jumuiya yetu pia tuliweza kuitisha kikao cha kujadili na kuchangia maoni ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kikao hicho kilihudhuriwa na msaidizi balozi na Mkuu wa utawala wa ubalozi wa Tanzania Rome, Mh.Salvator M.J.Mbilinyi. Kikao hiki kilikuwa na mafanikio makubwa kwani watanzania walipata maelezo ya kina na jinsi ya kuchangia maoni ya katiba mpya.
- Mwezi wa desemba 2012,Jumuiya ilipata mualiko wa kuhudhuria mkutano wa Chama cha Radicale italiani, kuchangia maoni kuhusu masuala ya wageni wahamiaji.
Matukio haya yote ni mafanikio ya Jumuiya yetu kwa kiasi kikubwa na kama nilivyoelezea kuwa matatizo yetu makubwa yaliyotukuta ni misiba, lakini tunamshukuru MwenyeziMungu kwa kutuwezesha kukusanya michango iliyofanikisha kusafirisha miili nyumbani, hili ni kati ya mafanikio makubwa ya Jumuiya ya Watanzania Italia tangu ilipoundwa rasmi na kupata matawi na uwakilishi sehemu mbalimbali mikoani . Jumuiya imefanya kazi kubwa sana ya kuwaunganisha Watanzania na kuhakikisha kuwa Watanzania wanakuwa pamoja katika matatizo na furaha.Vile vile kwa upande wa Wagonjwa tumeweza kuwashughulikia kwa kadiri ya uwezo wetu. Mwito wa 2013/2014:
Katika mwaka huu mpya napenda kuto mwito kwa Watanzania wote na wanajumuiya wa Jumuiya ya Watanzania Italia kama ifuatavyo:
- Natoa wito kwa Watanzania wote kujiandikisha kwenye Jumuiya ili tuwe na idadi kamili ya Watanzania, wapi wanaishi na anuani zao.Vilevile kwa walio na watoto pia ni muhimu kuwandikisha. Hii itatusaidia kwa mambo mbalimbali pamoja na kuwasiliana pale inapohitajika.
- Matawi yote na wawakilishi wa jumuiya ya Watanzania Italia lazima kufuata taratibu za katiba yetu, kuwa na mikutano ya viongozi na Watanzania wote katika sehemu zao. Viongozi wa jumuiya wakae na kupanga taratibu za mikutano na tarehe kwa mwaka huu wa 2013. Ratiba za vikao ziwafikie Watanzania wote.
- Ndugu zangu Watanzania, kama mnavyojua Jumuiya yetu tunaiendesha kwa kujitolea, kwa hiyo nazidi kusisitiza zaidi kuwa kila Mwanajumuiya ni wajibu wake kutoa mchango wa kila mwaka wa Euro 20,00 kwa ajili ya shughuli za uendeshaji na kazi za Jumuiya.
- Na kwa wale ambao bado hawajajiandisha tafadhali mfike katika ofisi zetu,au muwasiliane na katibu au mwakilishi wetu wa eneo lako ili uweze kupata fomu na maelezo zaidi ya kujiandikisha.
- Utaratibu wetu wa kufungua matawi ya jumuiya utakuwa na umuhimu mkubwa kwa kipindi hiki cha 2013/2014 kutokana na maombi mengi ambayo tumeyapokea kutoka kwa Watanzania mbalimbali walioko mikoa mingine.
- Wanajumuiya wazingatie mahudhurio ya vikao vyote vya jumuiya ili tuweze kujadili mambo yanayotuhusu kwa pamoja na kuhudhuria vikao tunavyoalikwa na jumuiya za mataifa mengine na zile za wenyeji wetu Wataliani.
- Kila mwaka kutakuwa na mikutano miwili ya Jumuiya, itakayoshirikisha Watanzania wote, kukusanya maoni na kutoa maelezo na taarifa muhimu zinazohusu watanzania wote. Kila mmoja wetu ana wajibu wa kuhudhuria vikao hivi muhimu. Vikao hivi viwili vimetofautiana hivi: Kikao cha kwanza yaani mwanzoni mwa mwaka kitafanyika katika kila tawi la Jumuiya ya Watanzania Italia na kile cha pili ambacho ni kikubwa kitafanyika makao makuu ya jumuiya mjini NAPOLI. Ambacho kitakutanisha Watanzania wote kutoka kila mkoa wa Italia. Katika kikao hiki cha mwisho wa mwaka viongozi watatoa taarifa za maendeleo ya jumuiya kutoka matawi yote, pamoja na taarifa zote muhimu. Tarehe za vikao hivi zitatolewa rasmi na makao makuu ya Jumuiya.
Namaliza kwa kutumia nafasi hii kuwashukuru sana Watanzania wote kwa kuwa na moyo wa kujitolea kwa hali na mali, napenda kuwafahamisha kuwa michango yenu inatambulika na tunaithamini sana.
Jumuiya bado inahitaji msaada zaidi kwa hiyo nasisitiza sote tujitokeze katika kusaidia jumuiya hii ambayo ni chombo muhimu sana kwa Watanzania wote. Serikali yetu inalitambua hili na inathamini sana mchango wa Watanzania wote ughaibuni.( Tanzania Diaspora)
Nachukua nafasi hii kuishukuru serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mh. Raisi Jakaya Kikwete kwa kutoa nafasi kwa Wataalaam mbalimbali walioko ughaibuni (diaspora) kushiriki katika ujenzi wa nchi yetu kwa kutuma CVs zao ili waweze kupata mikataba ya kazi katika sekta mbalimbali.
Ndugu zangu hii ni nafasi nzuri sana kwetu katika kushiriki kikamilifu kujenga nchi yetu naamini tunayo mengi mazuri ya kuchangia katika ujenzi wa nchi yetu, hima wote walio na ujuzi kupeleka maelezo yao kwani nafasi hii inaonyesha jinsi gani Serikali yetu inavyothamini Watanzania waliopo nje.
Mwisho Nawatakia kila la heri na mafanikio katika mwaka huu mpya wa 2013.
Mungu ibariki Jumuiya yetu, Mungu ibariki TANZANIA!